Jumamosi, 20 Aprili 2024

CHOMBO MAALUM CHANUKIA KUSHUGHULIKIA RUFAA ZA WAFANYAKAZI KUHUSU FIDIA

  • Waajiri ambao hawajasajiliwa, kuwasilisha michango kwa wakati kukiona

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Kigoma

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi ameridhia kuanzishwa kwa chombo maalumu kitakachokuwa kinashughulikia rufaa za wafanyakazi baada ya maamuzi ya fidia yanayotolewa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

 

Mhe. Ndejembi ametoa ridhaa hiyo leo tarehe 20 Aprili, 2024 alipokuwa akifunga Kikao Kazi kujadili sheria za kazi kilichokuwa kinafanyika kwenye Ukumbi wa Lake Tanganyika mkoani hapa kilichowaleta pamoja Majaji na Watendaji wa Mahakama na Menejimenti ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi.

 

 “Nimesikia kilio hiki cha kuwa na chombo maalum kwa ajili ya kushughulikia masuala haya ya fidia hasa kwa wale ambao watakuwa hawajaridhika na maamuzi yanayotolewa. Naamini kwenye kikao kichacho tutakapokutana tutakuwa tumeanza kupiga hatua kuelekea kuwa na chombo hiki,” amesema.

 

Waziri Ndejembi amebainisha kuwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, kwa kushirikiana na Kurugenzi ya Hifadhi ya Jamii iliyochini ya Wizara anayoisimamia, wanaendelea na uchambuzi wa maboresho ya Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi.  

 

Amesema kuwa uchambuzi huo unatarajiwa kuja na andiko kuhusu kuanzishwa kwa chombo maalum cha kusimamia rufaa zinazotokana na masuala ya hifadhi ya jamii badala ya utaratibu wa sasa wa rufaa hizo kuwasilishwa kwa Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi.  

 

“Ni matumaini yangu kuwa katika kikao kazi hiki, mmepata fursa ya kutoa maoni zaidi kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utekelezaji na uboreshwaji wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi,” amesema.

 

Mhe. Ndejembi ameeleza pia kuwa Serikali kupitia Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi imefikia uamuzi wa kutoa mafunzo kutokana na kutambua umuhimu na nafasi ya Majaji na Watendaji wengine wa Mahakama katika mchakato wa kutoa haki. 

 

Amesema kwamba mchakato huo, pamoja na mambo mengine, unahusisha namna ya kushughulikia madai ya fidia kwa wafanyakazi wanaogua au kuumia wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao ya kazi kwa mujibu wa mikataba yao. 

 

Aidha, Waziri huyo ameeleza kuwa mchakato huo pia unahusisha namna ya kupata haki katika mamlaka ya rufaa pale mfanyakazi hatakuwa ameridhika na maamuzi ya fidia kwa mujibu wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi.

 

Hivyo, akabainisha kuwa pamoja na gharama zinazotumika katika kuendesha kikao kazi hicho ilikuwa ni lazima kifanyike ili kuimarisha ushirikiano na kujenga uelewa wa pamoja katika kusimamia madai yanayohusiana na fidia kwa wafanyakazi.  

 

“Nimefurahi kwa jinsi mlivyotumia kikao hiki pamoja na vilivyofanyika awali kufanya uchambuzi wa sheria za kazi, hususani ile ya Fidia kwa Wafanyakazi na kutoa maoni ya kuboresha sheria hiyo,” amesema.

 

Mhe. Ndejembi alitumia fursa hiyo kuushukuru Uongozi wa Mahakama kwa kukubali na kuwaruhusu Majaji na Watendaji wa Mahakama kushiriki kikao kazi hicho muhimu kinacholenga kujengeana uwezo pamoja na kubadilishana uzoefu katika masuala ya fidia kwa wafanyakazi na sheria za kazi kwa ujumla wake.

 

Hata hivyo, Waziri huyo aliusisitiza Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kuongeza bidii na kasi zaidi katika kushughulikia madai kwa wateja wao ili waendane na ile kauli mbiu ya Mfuko ya “Fidia Stahiki na kwa Wakati.” 

 

Kadhalika, aliwataka kuongeza bidii katika kuwabana na kuwashughulikia Waajiri wote wanaokaidi matakwa ya Sheria kwa kutojisajili na kutowasilisha michango kwa wakati. 

 

Awali, akimkaribisha Waziri kufunga Kikao Kazi hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, alieleza kuwa jukwaa hilo alimekuwa la daraja la juu kuliko yote ambayo yamewahi kufanyika.

 

Alisema kuwa kikao cha kwanza kilifanyika Bagamoyo kwa kuhusisha Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi pamoja na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi Kanda ya Dar es Salaam na Pwani na kufuatiwa na kikao cha pili kilichofanyika Mwanza kwa kuhusisha Kanda zote zinazotoka Kanda ya Ziwa, yaani Shinyanga, Musoma, Mwanza na Bukoba.

 

Mhe. Dkt. Mlyambina alimweleza Waziri kuwa baada ya kikao cha Mwanza walielekea Arusha na kuhusisha Mikoa ya Tanga, Manyara, Kilimanjaro na Arusha kabla ya kuelekea Songea ambapo Kanda za Sumbawanga, Mbeya, Iringa na Songea yenyewe zilihusishwa.

 

“Leo tupo hapa Kigoma na tumewaleta wenzetu kutoka Morogoro, Dodoma, Tabora na Majaji wenzetu ambao hawakushiriki kwenye vikao vilivyopita kutoka Shinyanga, Iringa na Sumbawanga,” amesema.

 

Amebainisha pia kuwa Kikao Kazi hicho kimekuwa, kwa namna ya kipekee, na sura ya muungano kufuatia ushiriki wa Jaji wa Mahakama Kuu na Mwenyekiti wa Mahakama ya Kazi Zanzibar, Mhe. Aziza Idd Sued, ambaye ametoa uzoefu mzuri kuhusu masuala ya kazi na wamejisikia kuwa Taifa moja.

 

Jaji Mfawidhi alimweleza Waziri kuwa uwepo wa vikao kazi kama hivyo ni muhimu kwani vinawajengea uwezo zaidi katika kuelewa vema kuhusu maeneo ambayo mfanyakazi anaweza kulipwa fidia, vigezo vinavyotumika, hatua stahiki na taratibu mahsusi katika ufuatiliaji wa madai ya fidia kwa wafanyakazi.

 

“Pia vinatusaidia kuainisha baadhi ya mapungufu yaliyopo katika sheria husika. Mahakama na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ndiyo wanaotafsiri sheria. Hivyo, tunapowakusanya watumishi hawa kwa pamoja inakuwa rahisi kujua sheria hii katika kuipima inakuwa na mapungufu yapi na namna gani ya kuondokana nayo,” amesema.

 

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba, alimweleza Waziri kuwa jambo kubwa moja lililosisitizwa na washiriki wakati wa majadiliano ni kuanzishwa kwa chombo mahususi cha kushughulikia rufaa zinazotokana na maamuzi yanayofanywa na taasisi za hifadhi ya jamii.

 

“Suala hili limejitokeza katika vikao kazi vyote vilivyofanyika. Sisi kama Bodi ya Wadhamini tumepokea ushauri huu na tayari tuliuwasilisha katika Wizara yako kwa hatua zaidi za utekelezaji ambapo mtangulizi wako aliagiza Kurugenzi ya Hifadhi ya Jamii kuanza kuaanda andiko la mapendekezo ya utekelezaji wake,” alisema.

 

Bw. Humba alisema kuwa yeye kama Mwenyekiti wa Bodi anaahidi kuendeleza ushirikiano na Mahakama na Taasisi nyingine zenye dhamana ya kutekeleza sheria za kazi kwa lengo la kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi akisisitiza jambo alipokuwa anafunga Kikao Kazi kilichowaleta pamoja Majaji na Wadau mbalimbali kujadili sheria za kazi.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akiwasilisha salamu za Mahakama kwenye Kikao Kazi hicho.


Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba akifafanua jambo wakati wa hafla hiyo.


Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Dkt. John Mduma akieleza jambo wakati wa Kikao Kazi hicho.

 

Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Zanzibar, Divisheni ya Kazi, Mhe. Aziza Idd Sued (kushoto) akiwa na Majaji wa Mahakama ya Tanzania kwenye Kikao Kazi hicho.




Sehemu ya Majaji kutoka Kanda mbalimbali za Mahakama Kuu ya Tanzania (juu na chini) wakiwa katika Kikao Kazi hicho.



Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Wadau (juu na chini) wakishiriki kwenye Kikao Kazi hicho.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kutoka Kanda mbalimbali na Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Kazi Zanzibar.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu kutoka Kanda mbalimbali na Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Kazi Zanzibar.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi na watumishi wa Mahakama waliokuwa wanahudhuria Kikao Kazi hicho.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Menejimenti ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi.





Ijumaa, 19 Aprili 2024

MAJAJI WASHAURI SHERIA KUPANUA UWIGO WA MAFAO KWA WAFANYAKAZI

Na Aidan Robert-Mahakama, Kigoma

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. Eliamani Laitaika ameshauri sheria inayosimamia fidia kwa wafanyakazi kuongeza uwigo wa mafao, ikiwemo kutoa fidia kwa wale wanaoathirika kiakiri wanapotekeleza majukumu yao.

 

Mhe. Laitaika ametoa ushauri huo leo tarehe 19 Aprili, 2024 alipokuwa akichangia mada kwenye Kikao Kazi kujadili sheria za kazi kinachofanyika kwenye Ukumbi wa Lake Tanganyika mkoani hapa.

 

“Ni vyema sheria ikatambua kulipa fidia kwa mtu ambaye anapata athari za kiakili kwani ni kiungo ambacho kinaathirika kwa kiwango kikubwa na hakionekani kwa mhanga, lakini uwezo wake kupungua au kufa kabisa na kukosa ufanisi katika kazi kutokana adha ya vifaa vya kielekroniki vinavyotumika mahala pa kazi na kutumia kwa muda mrefu,” amesema.

 

Amebainisha kuwa sheria ya fidia kwa wafanyakazi imetoa fidia pekee kwa mfanyakazi ambaye atapata ajali au kifo au ugonjwa pekee, wakati kwa maisha ya sasa wafanyakazi wengi wanatumia asilimia kubwa kwenye akiri.

 

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Majadiliano katika kikao hicho, amesema sheria ya sasa inayosimamia fidia kwa wafanyakazi inatoa changamoto kadhaa kwa baadhi ya vifungu hasa pale inapotekelezwa katika maamuzi mbalimbali.

 

Akiwasilisha mada yake katika kikao kazi hicho, Mkuu wa Huduma za Sheria wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Ibrahimu Siyovelwa, amesema kuwa Mfumo ni Tasisi ya Hifadhi ya Jamii iliyoundwa kwa mujibu wa Sheria kwa lengo la kushughulikia masuala ya fidia kwa wafanyakazi waliopo katika sekta ya umma na binafsi ambao wataumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi wanazozifanya kwa mujibu wa mikataba ya ajira zao na wategemezi wa mfanyakazi atakayefariki dunia kutokana na ajali au ugonjwa uliotokana na kazi.

 

Amesema kuwa ulipwaji wa mafao ya fidia unahusisha matukio ya ajali, ugonjwa au kifo yaliyotokea kuanzia tarehe 01, Julai 20216 na mpaka sasa. Bw. Siyovelwa amebainisha kuwa madai ya fidia yanapaswa kuwasilishwa ndani ya siku au kipindi kisichozidi miezi 12 tokea tukio husika lilipotokea au kugundulika. 


Aidha alibainisha kuwa Mfuko huo unatoa mafao ya huduma ya matibabu, fidia ya ulemavu wa muda, fidia ya ulemavu wa kudumu, malipo ya anayemhudumia mgongwa, huduma za utegemezi, msaada wa mazishi na malipo kwa wategemezi.

 

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tathimini Mfuko wa Hifadhi ya Jamii, Dkt. Abulsaalam Omary amesema wanafanya tathimini ya fidia kwa madhara ili kutoa fidia stahiki katika ulemavu wa kudumu na fao hilo pia hulipwa kwa mfanyakazi aliyepata ulemavu kwa kiasi ambacho kimeathiri uwezo wake wa kutimiza majukumu yake kazini.

 

Naye Bw. Rashidi Wabhike, Mkazi wa Kigoma ambaye ni mnufaika amesema hakika Mfuko huo umekuwa mkombozi wa maisha yake  baada ya kupata ajali ya shoti ya umeme alipokuwa akitekeleza majukumu wake kule mkoani Arusha alipopata ulemavu wa kudumu wa mguu wake wa kushoto.

 

Ameeleza kuwa aliondolewa kazini na baadaye Mfuko huo kuchukuwa jukumu baada ya kupokea taarifa ya mfanyakazi huyo kupata ajali, ambapo matibabu yake yote yalisimamiwa na Mfuko na hivi sasa anaendelea vyema baada kumwezesha kupata mguu wa bandia baada ya mguu wake halisi kuondolewa kutokana na kuharibiwa na shoti ya umeme.

 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dkt. Eliamani Laitaika, akisikiliza kwa makini maelezo ya muwasilisha mada mara baada ya kutoa ushauri kuhusu Sheria ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi katika kikao kazi cha kujadili sheria za kazi leo tarehe 19 Aprili, 2024 kinachafanyika katika ukumbi wa Lake Tanganyika Kigoma.


 

Mkurugenzi wa Huduma za Tathimini Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Dkt. Abulsalaam Omary, akiwasilisha mada katika kikao kazi hicho.





Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Abraham Siyovelwa, akisisitiza japo wakati akiwasilisha mada.


Naibu Msajili wa mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro, Mhe. Fadhili Mbelwa akiwasilisha hoja. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Gadiel Mariki na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora, Mhe. Pamela Mazengo.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Kigoma)

 

  

WANAFUNZI SHULE YA SEKONDARI MOROGORO WASHANGAZWA NA MABORESHO MAHAKAMANI


Na Evelina Odemba – Mahakama, Morogoro

 

Hivi karibuni Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Morogoro walitembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro ili kujifunza maboresho yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania katika kurahisisha shughuli za utoaji haki.

 

Wanafunzi hao walipokelewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo, ambaye aliwapa elimu ya muundo wa Mahakama na namna unavyoshirikiana katika kufanya kazi.

 

Mhe. Kallomo aliwaeleza wanafunzi hao namna Mahakama ya Tanzania imefanya maboresho katika miundombinu ya majengo, mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na namna huduma kwa mteja inavyotolewa.

 

“Nawapa elimu hii kwa manufaa yenu na kwa jamii nzima, ni imani yangu kuwa wote mliopata ufafanuzi huu mtaenda kuwa mabarozi wazuri katika jamii kuhusiana na namna ambavyo maboresho yaliyofanywa na Mahakama ya Tanzania yanavyomrahisishia mwananchi kupata haki” alisema.

 

Naye Kaimu Afisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Bw. Tofiki Sumbuo aliwapitisha wanafunzi hao katika mifumo ya inayotumiwa na Mahakama, jambo lililowavutia namna usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao unavyofanyika.

 

Kwa upande wake, Kiongozi wa Wanafunzi hao, Bi. Khadija Mrisho alisema kuwa wamevutiwa na namna ambavyo Mahakama ya Tanzania inavyofanya kazi na wamejifunza kuhusu mambo mengi na mazuri ambayo hapo kabla hawakuwahi kuyajua. 

 

Aliongeza kuwa wamevutiwa siku moja watakuwa sehemu ya mnyororo wa watoa huduma ya haki kwa wananchi mara watakapohitimu elimu yao.

 

Mwanafunzi mwingine, Nasma Wenzi alisdhangazwa na ukarimu ulioneshwa na watumishi kuanzia katika lango la kuingilia hadi katika maeneo mbalimbali waliyotembelea mahakamani hapo.

 

“Kipindi tunaingia getini tulikuwa na hofu ,tukidhania kila mtu ndani ya jengo hili ni mkali, lakini baada ya kupokelewa tumegundua kuwa watumishi ni wakarimu na wametuelekeza kwa upendo mpaka hofu tuliyokuwa nayo ikayeyuka na tukawa huru kuuliza maswali,” alisema.

 

Wakiwa kituoni hapa wanafunzi hao walipata fursa ya kutembelea Mahakama ya Watoto, Mahakama ya Wazi, Ofisi za wadau wa Mahakama pamoja na Ofisi ya TEHAMA.

 


 Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo akiwa katika picha ya Pamoja na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Morogoro ambao walitembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki ili kujifunza.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo akitoa elimu kwa Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Morogoro.


 

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo akiwaonesha Wanafunzi hao ofisi mbalimbali zilizopo ndani ya Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki.


 

Kaimu Afisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Bw. Tofiki Sumbuo akiwaonesha Wanafunzi hao baadhi ya mifumo inayotumiwa na Mahakama ya Tanzania.


 

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Morogoro wakiwa katika ukumbi wa Mahakama ya Wazi.


 


Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Morogoro wakisikiliza kwa makini elimu iliyokuwa ikitolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Morogoro, Mhe. Mary Kallomo walipotembelea jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Kigoma)

 

 

 

 

MAHAKAMA YA TANZANIA KIMBILIO LA WANANCHI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Kigoma

Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba ameupongeza uongozi wa Mhimili wa Mahakama, chini ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, kwa mageuzi makubwa ambayo yameifanya Mahakama ya Tanzania kuwa kimbilio la Wananchi.

Bw. Humba ametoa pongezi hizo leo tarehe 19 Aprili, 2024 alipokuwa anawasilisha salamu zake kwenye Kikao Kazi kujadili sheria za kazi kinachofanyika katika Ukumbi wa Lake Tanganyika mkoani hapa.

Kikao Kazi hicho ambacho kimeratibiwa na Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi kwa kushirikiana na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kinawaleta pamoja Majaji wa Mahakama Kuu kutoka Kanda mbalimbali na Mahakama Kuu Zanzibar na Wadau kutoka Mfuko huo na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi. 

Akizungumza wakati wa kutoa salamu zake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko amesema uongozi wa Mahakama umeipa heshima kubwa Mahakama ya Tanzania kiasi cha kuwafanya Wananchi kukimbilia mahakamani ili kupata haki stahiki wanapokabiliana na changamoto mbalimbali.

“Tunapenda, kwa kweli kukupa heshima ya hali ya juu. Mahakama kwa sasa hivi inaonesha ushirikiano mzuri sana. Huko nyuma kulikuwa na mashaka mashaka, raia walikuwa wanaiogopa Mahakama, Mahakama zenyewe zilikuwa zinatisha…

“…Lakini sasa ni tofauti sana, kwa malezi yako, Mahakama na Wananchi wanavuna mbivu na wanapenda kukimbilia mahakamani. Binafsi, nakushukuru sana,” Bw. Humba alimweleza Jaji Mkuu ambaye aliyekuwa Mgeni Rasmi kwenye ufunguzi wa Kikao Kazi hicho.

Katika salamu zake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ameeleza kuwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi ni Taasisi ya Hifadhi ya Jamii ulioanzishwa chini ya Kifungu cha 5 cha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi kwa lengo la kushughulikia masuala ya fidia kwa wafanyakazi wanaoumia au kufariki katika utekelezaji wa majukumu yao ya ajira.  

Amesema kwamba Mfuko huo ulianza kutekeleza majukumu yake tarehe 01 Julai, 2015 na ulipewa kipindi cha mpito cha mwaka mmoja kwa ajili ya maandalizi ya kulipa fidia na hivyo kuanza kulipa fidia rasmi tarehe 01 Julai 2016.

“Napenda kukuhakishia kuwa Mfuko unaendeshwa kwa ufanisi mkubwa na umepata mafanikio makubwa katika kutekeleza malengo yake. Tulipoanza mwaka 2016, tulilipa fidia kwa Wafanyakazi ya Shilingi za Kitanzania Bilioni 3.88. Mpaka kufikia mwaka 2016/2017 mfuko umelipa mafao ya Shilingi za Kitanzania Bilioni 23.58,” Bw. Humba alimweleza Jaji Mkuu.

Amebainisha pia kuwa michango ya Waajiri iliyokusanywa imeongezeka kutoka Shillingi za Kitanzania 68.40 bilioni kwa mwaka 2015/2016 hadi kufikia Shillingi za Kitanzania 86. 48 bilioni kwa mwaka 2022/2023.  

Kdhalika, Mwenyekiti wa Bodi ameeleza kuwa pamoja na mafanikio hayo, tathmnini ya uhai na uendelevu wa Mfuko iliofanywa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) inaonesha kwamba Mfuko unauhimilivu kwa kipindi cha miaka 30 ijayo.

“Hiki ni kitu cha kukilinda, Mifuko mara kwa mara inaanza vizuri, isipolindwa inapoteza njia,” alisema. Amebainisha pia kuwa Mfuko umekuwa na utaratibu wa kushughulikia madai ya wanufaika kwa wakati uliowekwa kisheria.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Dkt. John Mduma, akizungumza wakati wa Kikao Kazi, hicho alieleza kuwa shughuli za Mfuko haziwezi kukamilika bila kupata ushirikiano kutoka mahakamani.

Alieleza kuwa kwa sasa maamuzi wanayoyatoa yanaangaliwa na Waziri mwenye dhamana pale ambapo kunakuwepo na kutokuridhika kwa upande mmoja na suala hufikishwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi kama mhusika asiporidhishwa na maamuzi ya Waziri.

“Kwa hiyo, unaweza kuona jinsi Mahakama ya Tanzania inavyoingia katika masuala ya fidia. Pia huwa tunakutana katika kuamua masuala ya mirathi ambapo tunategemea maamuzi yanayotokewa na Mahakama,” alisema.


Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba akizungumza katika Kikao Kazi kinachofanyika mkoani Kigoma leo tarehe 19 Aprili, 2024.


Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Dkt. John Mduma akieleza jambo wakati wa Kikao Kazi hicho.


Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati). Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Dkt. John Mduma (wa pili kulia), Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu, Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile (wa kwanza kushoto) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba (wa kwanza kulia).


Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kutoka Kanda mbalimbali na Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Kazi Zanzibar.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu kutoka Kanda mbalimbali na Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Kazi Zanzibar wanaohudhuria Kikao Kazi hicho.


Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Viongozi na Watumishi wa Mahakama wanaohudhuria Kikao Kazi hicho.



Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Menejimenti ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi na Tume ya Uamuzi na Usuluhishi.

Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi kutoka Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi.

JAJI MKUU WA TANZANIA AHIMIZA MAZINGIRA BORA KAZINI

  •      Asema udanganyifu, kukosa umakini kunafilisi mifuko ya jamii

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Kigoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewahimiza waajiri nchini kuhakikisha maeneo ya kazi hayatoi mazingira ya ajali wala vifo kwa wafanyakazi.

Mhe. Prof. Juma ametoa rai hiyo leo tarehe 19 Aprili, 2024 alipokuwa anafungua Kikao Kazi kujadili sheria za kazi ambacho kimewaleta pamoja mkoani hapa Majaji na watumishi wengine wa Mahakama pamoja na Menejimenti ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi na Tume ya Uamuzi na Usuluhishi. 

“Mfuko huu unalindwa na sisi kwa kuangalia mazingira ya kazi. Tupunguze visababishi ambavyo vinaweza kuleta vifo, ajali katika maeneo ya kazi. Hilo ni somo ambalo ni muhimu, tukirudi tuanze kuangalia maeneo yetu ya kazi kama ni rafiki,” amesema.

Jaji Mkuu amebainisha kuwa amepata bahati ya kupitia Sheria ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, kifungu cha 3 (f), ingawa watekelezaji wakubwa ni mfuko, inawataka waajiri kuhakikisha maeneo ya kazi hayatoi mazingira ya ajali wala vifo kwa wafanyakazi.

Mhe. Prof. Juma amesema uwepo wa Kikao Kazi hicho ni muhimu kwani kitawafanya kuyaelewa vizuri mazingira ya kazi na kuleta uelewa wa pamoja wa sheria kati ya wafanyakazi na Watanzania kwa ujumla.

“Kikao kazi hiki pia ni nafasi kwa wadau kujadiliana kwa sababu sheria ni moja, lakini huwa kunakuwa na uelewa unaotofautiana, hivyo ikipatikana fursa ya kujadiliana kati ya mfuko na Majaji, Wasajili, Watendaji husaidia kufahamu sheria kwa undani zaidi,” amesema.

Jaji Mkuu amebainisha kuwa kazi ya mfuko itakuwa rahisi kama kutakuwepo na uelewa unaofanana na kuepusha matumizi ya kanuni za kiufundi zinazolenga kumnyima mfanyakazi haki zake na pia kuweka uwiano mzuri katika malipo.

Mhe. Prof. Juma amesema kuwa ukisoma sheria ya mfuko wa fidia kwa wafanyakazi inaeleza malipo yanayotolewa yasilenge kufilisi mfuko. Amesema mifuko mingi hufilisika kama kutajengekaa tabia za udanganyifu. 

“Ukosefu wa umakini, udanganyifu vyote vimechangia kuua mifuko ambayo ilikuwa na malengo mazuri sana. Tusipokuwa waangalifu, mfuko huu vile vile unaweza kukumbana na tatizo hili. Tukielewa vizuri mantiki ya kuanzishwa mfuko huu tutaufanya uwe endelevu na himilivu,” amesema.

Jaji Mkuu ametumia nafasi hiyo kuhimiza pia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika shughuli zote za kiutendaji ili Taasisi za kimahakama na Wadau wote ziweze kusomana, hatua itakayosaidia kuziba udanganyifu na kuufanya mfuko kuwa himilivu na fidia kupatikana kwa haraka.

Awali, akizungumza kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu kufungua Kikao Kazi hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambia alisema kuwa kumekuwa na vikao kazi vitano ambavyo vimefanyika baina ya Mahakama na Wadau wake Bagamoyo, Mwanza, Arusha, Songea na Kigoma.

Alibainisha kuwa jumla ya Viongozi na watumishi 290 wameshiriki katika Vikao Kazi hivyo, wakiwemo Majaji 70, Naibu Wasajili 33, Watendaji 11, Wadau 48, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi 32 na zaidi ya watumishi wa Mahakama 96.

Alibainisha kuwa katika Kanda ambazo wamefanya mafunzo, kuna mambo ambayo yamekuwa yakiibuliwa na washiriki kwa lengo la kuboresha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi na baadhi ya mapendekezo yaliyoibuliwa yameshaanza kufanyiwa kazi na mfuko.

Mhe. Dkt. Mlyambia alitola mfano suala la mtu ambaye anakuwa hajaridhika na uamuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kukata rufaa kwa Waziri na baadae kwenda katika Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi.

“Katika mafunzo yaliyopita imependekezwa kwamba katika kufupisha mlolongo wa kudai fidia, kuanzishwe Baraza (Tribunal) litakaloshughulikia rufaa zinazotokana na maamuzi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia na mifuko mingine ya jamii,” alisema.

Jaji Mfawidhi alibainisha kuwa baada ya mzunguko wa awali wa mafunzo hayo, atawasilisha taarifa jumuishi ikionesha mapungufu na mapendekezo yaliyoibuliwa na washiriki wa mafunzo.

Alibainisha pia kuwa mafunzo hayo yamekuwa na upekee kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo kuwa mafunzo ya kwanza kuendeshwa na Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na Mfuko wa Fidia kwa wafanyakazi na pia kuwa na sura ya muungamo ambapo Jaji mwenye dhamana kutoka Zanzibar amehudhuria.

Alisema kuwa mafunzo hayo yamekuwa na washirikin wengi zaidi wakiwemo Majaji wasioungua 20 kutoka Kanda za Morogoro, Iringa, Songea, Dodoma, Tabora, Shinyanga na Kigoma.

Jaji Mfawidhi alieleza pia kuwa washiriki wamejifunza mambo mengi nje ya jamii ya Kigoma, ikiwemo kujua Ziwa Tanganyika limeundwa na sam aki wawili ambao ni Tanga mwenye uwezo wa kuruka juu zaidi na Nyika mwenye shoti za umeme ambaye ili kuweza kumwanda kama kitoweo ni lazima achunwe Ngozi yake.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anafungua Kikao Kazi kujadili sheria za kazi leo tarehe 19 Aprili, 2024 mkoani Kigoma.



Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambia akibainisha mambo fulani kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu kufungua Kikao Kazi hicho.


Sehemu ya Majaji kutoka Kanda mbalimbali za Mahakama Kuu ya Tanzania (juu na chini) wakiwa katika Kikao Kazi hicho.

 

 Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Zanzibar, Divisheni ya Kazi, Mhe. Aziza Idd Sued (kushoto) akiwa na Majaji wa Mahakama ya Tanzania kwenye Kikao Kazi hicho.


 

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Wadau (juu na chini) wakishiriki kwenye Kikao Kazi hicho.

Wadau na watumishi wa Mahakama (juu na chini) wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi uliofanywa na Jaji Mkuu wa Tanzania.

Picha na Aidan Robert-Mahakama Kigoma